Wadau wa DART wafanya ukaguzi wa ujenzi wa miundombinu awamu ya tatu
Wadau wanaoshiriki utekelezaji wa Mradi wa Mabasi Yaendayo Haraka (BRT) Awamu ya Tatu Jumanne walifanya ukaguzi wa kina wa miundombinu ya mradi huo ili kutathmini kiwango cha ukamilishaji wa vituo na mifumo ya uendeshaji katika ushoroba wenye urefu wa kilometa 23.6.
Ukaguzi huo ulianza katika eneo la Posta Mpya katikati ya Jiji la Dar es Salaam na uliwakutanisha wawakilishi kutoka Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka-DART, TANROADS, Sinohydro Corporation Limited, SMEC International pamoja na wadau wengine wanaoshiriki utekelezaji wa mradi huo.
Akizungumza wakati wa kuanza kwa ukaguzi huo, Mkurugenzi wa Maendeleo ya Usafirishaji wa DART, Mhandisi Ezron Kilamuhama, alisema wadau hao walifanya ukaguzi huo ili kuhakiki utekelezaji wa masuala yaliyobainishwa katika ukaguzi wa pamoja uliofanyika Machi 2026.
"Lengo la ukaguzi huu lilikuwa kupitia orodha ya maeneo yaliyobainishwa katika tathmini ya Machi 2026 na kuthibitisha kuwa mapendekezo yote yaliyotolewa yalikuwa yamefanyiwa kazi kabla ya kukabidhiwa miundombinu na baadae kuanza kwa huduma," alisema Mhandisi Kilamuhama.
Alisema timu hiyo ilikagua vipengele muhimu vya uendeshaji katika kila kituo ikiwemo vibanda vya tiketi, vyumba vya TEHAMA na mifumo ya umeme wa dharura, njia za nyaya za TEHAMA, vyumba vya UPS, mabango ya majina ya vituo, kazi za umeme na umaliziaji wa sakafu.
Wadau hao walikagua vituo vyote 33 vya Awamu ya Tatu vikiwemo Posta A, Posta B, CBE, Peacock, Mnazi Mmoja, Kamata, Banda la Ngozi, Kiuta, Sigara, TAZARA na Mchicha pamoja na vituo vingine vinavyoelekea Gongolamboto na Buguruni.
Katika ukaguzi huo, timu ilithibitisha kuwa sehemu kubwa ya miundombinu ilikuwa imekamilika na ilikuwa tayari kwa matumizi. Mifumo ya umeme, mawasiliano pamoja na kazi za umaliziaji wa vituo ilibainika kukidhi viwango vilivyowekwa.
"Tulibaini kuwa sehemu kubwa ya kazi za ujenzi zilikuwa zimekamilika kwa mujibu wa viwango vya mradi na shughuli zilizokuwa zimesalia zilikuwa chache sana," alisema Mhandisi Mkuu wa Sinohydro Corporation Limited, Zhang Cheng.
Ukaguzi huo pia ulibaini kuwa vifaa vya UPS vilikuwa bado havijafungwa katika vituo husika. Wadau wa mradi walieleza kuwa vifaa hivyo vingefungwa karibu na muda wa kuanza kwa huduma ili kulinda mifumo na kuhakikisha ufanisi wake.
"Mifumo mingi ya TEHAMA na umeme ilikuwa tayari imewekwa na kufanyiwa majaribio kwa mafanikio. Vifaa vya UPS vitafungwa karibu na muda wa kuanza kwa huduma za mabasi," alisema Dk. Ndyetabura Hamisi, Mshauri wa Umeme na TEHAMA kutoka SMEC International.
Kwa mujibu wa maafisa wa mradi, ushoroba wa Awamu ya Tatu unaanzia katikati ya jiji kupitia Mitaa ya Azikiwe na Maktaba, Barabara ya Bibi Titi na Barabara ya Nyerere kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere hadi Gongolamboto.
Tawi jingine linaanzia Kituo Kikuu cha Gerezani kupitia Mtaa wa Lindi, Shaurimoyo na Uhuru hadi Buguruni ambapo linaungana na Barabara ya Mandela na Barabara ya Nyerere katika makutano ya TAZARA. Mhandisi Kilamuhama alisema mradi huo utaimarisha kwa kiasi kikubwa usafiri wa umma na kuunganisha kwa ufanisi zaidi awamu mbalimbali za mfumo wa DART mara baada ya kuanza kwa huduma.
