Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka

"Usafiri wa Umma Nadhifu"

DART Logo
DART kusimika mfumo nadhifu wa kuongozea magari
20 Sep, 2023
DART kusimika mfumo nadhifu wa kuongozea magari

Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka (DART)  inatarijia kujenga na kusimika mfumo nadhifu wa kuongozea magari (Intelligence Transportation system – ITS) ndani ya miezi 14 kutoka sasa.

Hayo yamebainishwa na Mtendaji Mkuu wa DART, Dr. Edwin Mhede wakati wa mkutano wa kwanza na Wakandarasi waliopewa jukumu la ujengaji na usimikaji wa mfumo huo.

Katika mkutano huo uliofanyika katika hoteli ya Sea Cliff Dar es salaam Septemba 20, 2023 Dr. Mhede alisema mfumo huo ulihitajika toka mwanzoni wa huduma kuanza na kwamba wamekubaliana na wakandarasi hao kuhakikisha wanakamilisha kazi hiyo ndani ya muda waliokubaliana na ikiwezekana iwe chini ya hapo.

Dr. Mhede amesema mfumo huo nadhifu wa kuongozea magari, utasaidia kutoa huduma bora kwa wakati kwani kupita mfumo huo DART wataongoza magari kidigitali kwa kufahamu magari mangapi yanahitajika mahala gani na kwa muda gani.

“tunaamini katika  majira kama haya mwakani mfumo wa ITS utakua tayari umeshafungamanishwa na mifumo mingine na tutakua na operesheni control centre yetu  ambayo itarahisisha kuona kila kinachofanyika kwenye mfumo na kuwa na usafiri ambao ni wa kisasa na nadhifu kwa usalama wa watumiaji”

Dr. Mhede aliongeza kuwa mfumo huo pia utaisaidia DART kuzidisha usalama kwa abiria kwani utakuwa ukiangaza vitendo vyote viovu vinanavyotokea katika Mfumo wa Mabasi Yaendayo Haraka na ndani mabasi na hivyo kuchukua hatua kwa haraka nakwa  wakati ili kudhibiti.

“Mfumo wa ITS ni muhimu sio tu kwenye upangaji wa ratiba lakini pia ni kwa kuhakikisha usalama kwa sababu kutakua na uwezekano wa kuona kila kinachoendelea wakati wa endeshaji”

Aidha Dr. Mhede amesema mfumo huo nadhifu wakuongeozea magari utafungamanishwa na mifumo mengine ukiwemo Mfumo wa serikali wa ukusanyaji nauli (AFCS) unaotumika hivi sasa katika mabasi yaendayo haraka. Amesema ufungamanishaji wa mifumo utaufanya usafiri wa mabasi yaendayo haraka kuwa usafiri wa kisasa na nadhifu.

“Duniani kote iwe usafiri wa umma au usafirishaji wa mizigo, wanatumia mifumo ya ITS. Tofauti pekee ya mfumo wetu wa ITS na mingine ni kwamba sisi haitokua ITS inaojisimamia peke yake, sisi tutakua na ITS  ambayo imefungamanishwa na mifumo mingine ya usimamizi wa usafiri wa umma hapa Dar es Salaam”

Jukumu la kujenga na kusimika mfumo nadhifu wa kuongozea magari linatekelezwa na mkandarasi kutoka Hispania Kampuni ya IDOM ikishirikiana na Kampuni ya AES ya nchini Tanzania.